Tuesday, September 7, 2010

01

01

Tao inayoweza kuelezewa siyo Tao ya milele.
Jina linaloweza kutajwa kama jina sio jina la milele.

Kisichowezekana kupewa jina ndicho kilicho milele, cha kweli.
Kupewa jina ndio mwanzo wa vitu vyote vilivyopo ulimwenguni.


Huru kutokana na matamanio
huigundua ajabu hii.
Ukidakwa na matamanio basi utakachokiona ni vitu vinavyoonekana kwa nje tu.

Lakini ajabu na dalili za kuwepo ni vitu vinavyoanzia kwenye chanzo kimoja.
Chanzo hicho huitwa giza.

Giza ndani ya giza,
lango kuu kuingia kwenye uelewa wa kila jambo.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

02

Wakati watu wanapoona baadhi ya vitu kama vinavyopendeza;
vitu vingine huonekana vinavyochukiza na vibaya.
Watu wanapoona vitu vingine ni vizuri,
basi vingine hugeuka vyenye sura mbaya.

Kuwa na kuwepo ni vitu viwili vinavyoumbana;
Ugumu na urahisi wa mambo ni vitu vinavyoungana mkono;
Refu na fupi hufafanuana;
Juu na chini hutegemeana;
Kabla na baadaye hufuatana.

Kwa hiyo mwalimu hufanza bila kufanya kitu chochote
na hufundisha bila kusema chochote.
Vitu huzuka na huviachia vije,
Vitu hutoweka na huviachia kwenda zake.
Huwa navyo lakini hamiliki,
hufanya mambo bila kutarajia chochote.
Na kazi yake ikishafanyika huisahau.
Ndio sababu kazi zake hudumu milele.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

03

03
Ukiwaheshimu watu wakubwa kupita kiasi au kupindukia,
Watu hukosa nguvu na uwezo.

Ukizipa mali thamani kuliko watu,
basi watu huanza kuiba na kuwa wezi.

Mwalimu huongoza kwa kupakua kwanza akili za watu zikabakia tupu,
na kisha huanza kujaza akilini
kwa kudhibiti matamanio yao na kuamsha utu, ubinadamu na hamasa zao.
Huwasaidia watu kupoteza kila kitu wanachojua, wanachokitamani na kuzusha kuchanganyikiwa miongoni mwa wale wanaodhani wanajua.

Anza kufanya mazoezi ya kutofanya kitu chochote na kila kitu kitajiendesha chenyewe kwa asili bila kasoro.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

04

Tao ni kama kisima cha maji,
Watu hukitumia, lakini watu hawachoti maji kikaisha;
Ni kama anga tupu tusiyoiona ambayo kumbe imejaa kila aina ya vitu.

Imejificha lakini siku zote ipo.
Sijui ni nani aliyeizaa,
lakini hakuna anayeishinda kwa umri !

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

05

Tao haifungamani na upande wowote,
Huzaa wema na wabaya,
Mwalimu naye hafungamani na yeyote,
huwakaribisha wote,
watukufu na wenye dhambi.

Tao ni kama kiriba:
kwa kawaida ni kitupu lakini kina uwezo wa kufanya kazi kubwa.
Kadri unavyoitumia ndivyo inavyofanya kazi zaidi.
Kadri unavyoizungumzia ndivyo unavyozidi kutoielewa zaidi.

Kaa na shilkilia papo hapo katikati .

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

06

Tao huitwa Mama Mkuu,
tupu lakini isiyomalizika,
huzaa dunia kadhaa zisizo na idadi.

Sikuzote iko ndani yako,
na unaweza kuitumia kwa namna yoyote utakayo.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

07

Tao haihesebaki, haina idadi na ni isiyo na mwisho.
Kwanini haina mwisho na haifi ?
Haina mwisho na haifi kwa sababu haikuzaliwa;
kwa hiyo haiwezi ikafa.
Kwanini haihesabiki ?
Haina matamanio ya kujinufaisha yenyewe;
Kwa hiyo ipo kwa ajili ya kila kiumbe duniani.

Mwalimu siku zote hubakia nyuma;
Na ndio sababu siku zote yuko mbele ya wengine.
Hujitenga na vitu vyote;
Na ndio sababu yeye na hivyo vitu vingine ni kitu kimoja.
Kwa sababu amejiachia kwa vitu vyote,
huwa hana anachokikosa.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

08

Lililo jema na bora kabisa duniani ni kama maji,
yanayolisha watu wote bila ya kujaribu kufanya hivyo.
Huwa inaridhika na sehemu za chini ambako watu huwa hawapendi,
Kwa hiyo ni kama Tao.

Katika makazi ishi karibu kabisa na ardhi;
Katika kufikiri, fikiria kilicho chepesi na rahisi kabisa;
Katika ugomvi tenda haki na kuwa mkarimu.
Katika kutawala usijaribu kudhibiti.
Katika masuala ya kazi, fanya kazi uipendayo.
Na katika masuala ya familia, jaribu kuwepo saa zote kwa marefu na mapana yote.

Unapotosheka na kuwa kile uicho,
Na wala haujilinganishi wala kushindana na mtu,
kila binadamu atakuheshimu !

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

09

Jaza bakuli lako hadi pomoni na kilichomo kitamwagika;
Endelea kunoa kisu chako na hatimaye kitakuwa butu.
Fukuzia fedha na usalama wako na hautaufungua moyo wala mkono wako.
Jali na lilia kukubaliwa na watu,
kama hawajakugeuza kuwa mtumwa wao.

Fanya yako, kisha chukua hatua moja nyuma. Tulia.

Ndiyo njia pekee ya kupata utulivu na amani.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

010

Unaweza kuilazimisha akili yako kuacha kutangatanga na kurejea kwenye asili yake ya kuwa kitu kimoja ?
Je, uanweza kuufanya mwili wako uwe teketeke kama wa kitoto kichanga ?
Unaweza kuusafisha mwoneko wako wa ndani hadi unakuwa huoni kitu kingine ila mwanga ?
Unaweza kuwapenda watu na kuwaongoza bila ya wewe kutaka kuwaamlia kila kitu ?
Je, unaweza kuyashughulikia mambo yote muhimu kwa kuyaachia mambo yajiongoze yenyewe ?
Je, unaweza kuiacha nyuma akili yako ili uweze kuelewa kila kitu ?

Kuzaa, kutunza na kukimu,
kuwa nacho bila ya kumiliki,
kufanza bila kutarajia kitu,
kuongoza bila kudhibiti,
hakika hii ndio adili aali kuliko zote.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

011

Huwa tunaziunganisha spoki na gurudumu lakini ni tobo lililopo katikati ndilo linalolifanya gurudumu kutembea.

Huwa tunatengeneza vyungu kwa umbo la duara na nje kukapendeza sana,
lakini ni shimo tupu lililo katikati ndilo lenye thamani na ndilo linalohifadhi humo ndani chochote kile tunachotaka kukihifadhi.

Tunatumia miti au mbao pamoja na mawe na matofali kujengea nyumba.
Lakini kinachohitajika ni nafasi iliyomo ndani ya nyumba ili kuishi humo ndani.

Huwa tunafanya kazi na vilivyopo lakini ni vile visiopo ndivyo tunavyovitumia.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

012

Rangi huwa zinapofua macho,
Na sauti huleta uziwi.
Viungo huwa zinafifisha ladha kwenye ulimi.
Mawazo hudhoofisha akili.
Matamanio huukausha moyo.

Mwalimu huiangalia dunia, lakini huamini zaidi anachokiona ndani yake.
Huruhusu vitu kuja na kuondoka.
Moyo wake ni wazi kama vile anga ilivyo.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

013

Mafanikio ni hatari kama vile kushindwa,
Matumaini hayana kina kama uoga usivyo na kina pia.
Ina maana gani kusema mafanikio ni hatari kama kutofanikiwa ?
Kama unapanda ngazi kwenda juu au kushuka chini nafasi yako wakati wote ni ya wasiwasi.
Unaposimama kwa miguu yako miwili,
wakati wote utakuwa na balansi ya uhakika.
Nini maana ya matumaini na uoga vyote kutokuwa na kina sana ?
Matumaini na uoga ni viinimacho ambavyo vyote hutokana na mtu kutanguliza kufikiria nafasi yake kuliko kitu kingine,
Tutakapoiona nafsi kama sio nafsi yetu tu je, kutakuwa na sababu ya kuogopa kitu chochote?

Ione dunia nzima kama ndiyo nafsi yako.
Kuwa na imani na mambo kama yalivyo.
Ipende dunia kama unavyoipenda nafsi yako,
kisha utaweza kuviangalia vitu vingine vyote.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

014

Tazama, na hutakiona.
Sikiliza, na hutosikia kitu.
Jaribu kukikamata na hutoweza kukishika.

Kwa juu hakina mwangaza,
Kwa chini hakina kiza.
Bila umbo, bila jina
hatimaye hurejea katika milki ya kisichokuwepo.

Umbo linalojumuisha maumbo yote,
Taswira bila taswira,
Gumu kueleweka kupita ukomo wa dhahnia zote.

Kutana nayo na hutoona mwanzo wake;
ifuate na hutofika mwisho wake.
Huwezi ukaijua, lakini unaweza ukawa ndiyo yenyewe, bila kujua katika maisha yako ya kawaida ya kila siku.
Tambua tu kwanza ni wapi utokako
Hiki ndio kiini cha busara.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

015

Walimu wa kale walikuwa weledi na werevu mno.
Busara yao ilikuwa isiyo na kina.
Hakuna njia tunayoweza kuelezea, tunachoweza kueleza ni mwonekano wao wa nje tu.

Walikuwa waangalifu kama mtu aliyekuwa anakanyaga juu ya barafu iliyoko juu ya mto anaouvuka.
Waangavu kama askari katika nchi ya adui.
Wenye heshima kama wageni.
Majimaji kama barafu inayoyeyuka.
Inayoweza kuchongwa kirahisi kama kipande cha mti.
Kikaribishacho kama bonde.
Kinachoonekana wazi kama glasi ya maji.

Je, una subira ya kungoja mpaka tope lako limetulia na maji yamekuwa safi na meupe ?

Je unaweza kutulia hadi pale ambapo kitendo sahihi kinapoanza chenyewe ?

Mwalimu hatafuti kufanikisha mambo yake.
Na kwa kuwa hatafuti na hatarajii kitu chochote, yupo wakati wote na anaweza kukaribisha vitu vyote.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

016

Toa mawazo yote katika akili yako.
Acha moyo wako uwe katika amani.
Angalia misukosuko ya viumbe, lakini tafakari kurudi kwao.

Kila kiumbe katika dunia hii hurudi kwenye asili yake.
Kurudi kwenye chanzo chako ni utulivu.

Ikiwa hukijui chanzo chako basi huweweseka katika mtafaruku na huzuni.
Unapofahamu ni wapi unakotoka hujikuta mvumilivu, usiyevutwa na lolote, unayeshangazwa na mwenye moyo wa huruma kama nyanya,
mtukufu kama mfalme,
ukijitumbukiza katika maajabu ya Tao,
unaweza kupambana na lolote maisha yanachokuletea, na kifo kikija kinakukuta uko tayari.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

017

Mwalimu anapotawala watu
wengi wao huwa hata hawajui kama yupo.
Anayefuatia ni kiongozi anayependwa na watu wake.
Kisha anayefuatia, ni yule anayeogopwa na watu wake.
Kiongozi ovyo zaidi ni yule anayechukiwa na watu wake.

Kama huwaamini watu wako,
basi unawafanya wawe watu wasioaminika.

Mwalimu hazungumzi, hutenda.
Kazi yake inapokamilika watu husema:
" Ajabu, tumefanya mambo yote haya sisi wenyewe !"

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

018

Tao adhimu inaposahaulika,
wema na ucha Mungu huonekana.
Uwezo wa kiakili unapopungua,
werevu na maarifa hupatikana.
Panapokosekana amani katika familia, upendo katika familia huanza.
Nchi inapoingia katika machafuko,
mbegu za uzalendo huanza kupandwa.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

019

Tupilia mbali utakatifu na busara,
na watu watakuwa na furaha mara mia zaidi.
Tupilia mbali unyoofu na sheria,
na watu watafanya kilicho sahihi.
Tupilia mbali viwanda na faida,
na wezi hawatakuwepo tena.

Kama hivi vitatu havitoshi,
Basi kaa katikati ya mdurara
na kisha achia kila jambo kufuata mkondo wake.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]

Monday, September 6, 2010

020

Acha kufikiri, umalize matatizo yako.
Nini tofauti kati ya ndiyo na hapana ?
Nini tofauti kati ya kufanikiwa na kutofaulu ?
Je, ni lazima wewe uthamini wanavyothamini watu wengine ?
Uepuke kile wengine wanachotaka kukiepuka ?
Uzandiki ulioje huu ?

Watu wengine wanasisimka kama vile wako kwenye gwaride.
Mimi peke yangu ndiye nisiyejali,
Mimi mwenyewe ndiye nisiyeonesha ishara yoyote,
kama vile mtoto mchanga kabla hajatabasamu.

Watu wengine wana kila kitu wanachokihitaji;
Mimi peke yangu ndiye nisiye na chochote.
Mimi peke yangu ndiye ninayetangatanga,
kama vile sina kwangu.
Ni kama mpumbavu, akili yangu haina kitu.

Watu wengine wote wanang'ara
Isipokuwa mimi peke yangu ndiye mwenye weusi wa giza.
Watu wengine wamenolewa,
mimi peke yangu ndiye butu.
Watu wengine wana sababu, mimi peke yangu ndiye nisiyejua.
Ninaelea kama wimbi baharini,
Ninavuma bila lengo kama upepo uvumavyo.

Ni tofauti na binadamu wa kawaida,
Ninanyonya kutoka matiti ya mama wa mama wote.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

021

Mwalimu hupumzisha akili yake daima,
Sikuzote yuko pamoja na Tao;
hili ndilo linalompa nuru aliyokuwa nayo.

Tao huwa haikamatiki,
vipi akili zake ziwe pamoja na Tao.
Kwa sababu huwa hang'ang'anii dhana au wazo lolote liwalo.

Tao ni kiza na isiyo na mwisho,
Itamfanyaje yeye awe na nuru ?
Kwa sababu huiachia kufanya hivyo.

Kabla ya wakati na nafasi kuwepo,
Tao ipo.
Iko juu ya kuwa na kutokuwepo.
Ninajuaje hili ni kweli ?
Ni kwa kukiangalia kile kilicho ndani yangu nami nikakikubali.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

022

Ukitaka kuwa mkamilifu,
acha kwanza uwe vipande vipande.
Ukitaka unyooke,
acha kwanza upinde pinde.
Ukitaka uwe umejaa,
acha kwanza uwe tupu.
Ukitaka uzaliwe upya,
acha kwanza ufe.
Ukitaka upate kila kitu duniani,
acha kwanza utoe kila kitu ulicho nacho sasa.
Mwalimu anapokaa kwenye Tao,
basi huwa anakuwa mfano wa kuigwa na viumbe wote duniani.
Kwa sababu huwa hajioneshi,
basi watu huiona nuru yake.
Kwa sababu hana chochote cha kuthibitisha,
basi watu wanaamini maneno yake.
Kwa sababu hajijui yeye ni nani,
watu hujitambua wenyewe kupitia kwake.

Kwa sababu akilini hana malengo yoyote,
kila kitu anachofanya hufanikiwa.

Walimu wa zamani waliposema:
" UKitaka upate kila kitu, basi achia kila kitu, "
hawakuwa wakisema maneno matupu.
Ni pale unapoishi kama Tao tu ndipo unapoweza kuwa kweli ni wewe mwenyewe na sio kinyago cha Mzungu, Mmarekani, Mwarabu, Mchina au mtu mwingine au nyani mtu kwa wengine.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

023

Jieleze kwa ukamilifu, na kisha kaa kimya.
Kuwa kama vile nguvu za maumbile:
upepo ukipuliza, upo tu upepo;
mvua inaponywesha; ipo tu mvua;
mawingu yakishapita
basi jua huonekana.

Ukifungua moyo na akili zako kwa Tao,
wewe unakuwa ni mmoja na Tao,
na unaweza kuikumbatia yote kikamilifu.
Ukifungua moyo na akili yako kwa mitazamo ya ndani na nje;
basi unakuwa wewe mwenyewe mtazamo wa ndani na wa nje,
na unaweza ukalitumia hili kwa ukamilifu.
Unapofungua moyo na akili zako kwa hasara, unakuwa ni kitu kimoja na hasara na utalikubali hili moja kwa moja.

Ifungulie Tao sasa,
na kisha amini, fuata akili yako ya kuzaliwa na utajikuta unakiacha kila kitu mahala kinapostahili kuwepo.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

024

Anayesimama kwa vidole vyake vya mguu hawezi kuliweka umbo lake sawa.
Anayekimbilia kutaka kwenda mbele zaidi , huwa haendi popote.
Anayekazana kung'ara na kuwashinda wengine huwa anafifisha mng'ao na nuru yake.
Anayejaribu kujieleza kuwa yeye ni nani hawezi kujua yeye ni nani hasa.
Aliyekuwa na mamlaka juu ya wengine, hawezi yeye mwenyewe kujipa nguvu na uwezo juu ya chochote.
Anayeng'ang'ana tu na kazi yake, hawezi kuunda chochote cha maana kitakachodumu duniani.

Ukitaka kuwa kitu kimoja na Tao,
Timiza wajibu wako, kisha sahau ulichokifanya na ondoka nenda zako.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

025

Palikuwa na kitu kisichokuwa na umbo na kilichokuwa safi kabisa kabla ulimwengu haujazaliwa.

Ni tulivu. Tupu. Pweke. Isiyobadilika. Isiyo na idadi.Inayokuwepo milele. Ni mama wa ulimwengu.
Kwa kukosa jina lingine linalofaa zaidi,
nimeamua kuiita Tao.

Hutembea katika kila kitu, nje na ndani na kisha hurudi kwenye asili ya vitu vyote.

Tao ni muhimu.
Ulimwengu ni muhimu.
Ardhi ni muhimu.
Mtu ni muhimu.
Hizi ndizo nguvu kuu nne muhimu maishani.

Mtu huifuata ardhi,
na ardhi huufuata ulimwengu
Na ulimwengu unaifuata Tao,
Wakati Tao hujifuata yenyewe tu.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

026

Kitu kizito ndio mzizi wa kilicho chepesi,
Kisichotembea ndio mwanzo wa mienendo yote.

Ndiyo maana Mwalimu husafiri siku nzima bila kuondoka pale alipo.
Licha ya uzuri wa vile vinavyomzunguka siku nzima huwa katulia alipokaa.

Kwanini Bwana wa nchi awe na kiherehere na kujirahisisha kama mjinga ?

Ukijiachia ukawa unapeperushwa mbele na nyuma hujikuta huna mizizi yoyote.

Ukiafiki, kutotulia kuanza kukutembeza huku na huko basi utapoteza mawasiliano na kile wewe ulicho. Hutokuwa ni wewe mwenyewe ila kitu kingine kabisa.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

027

Msafiri mzuri huwa hana mipango ya kudumu ma wala hana haraka ya kufika.
Mchoraji mzuri huachia hisia zake zimpeleke kokote kule zitakako.
Mwanasayansi bora huwa kajikomboa na dhana zote na kuacha akili zake wazi kukubali lolote lile liwalo.

Kwa hiyo Gwiji wakati wote ule anawakaribisha wote na hakuna anayemkataa.

Yuko tayari kutumia hali yoyote ile iwayo na hawi mbadhirifu kwa chochote kile.
Hili huitwa kuuvaa nuru yote.

Kwani mtu mzuri ni nani zaidi ya kuwa mwalimu wa mtu mwovu ?
Kwani mtu mbaya ni nani zaidi ya kuwa kazi ya mtu mzuri ?
Ikiwa wewe hulielewi hili basi lazima utapotea, hata ukiwa na akili kiasi gani.
Hili ni mama wa siri zote duniani !

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

028

Mfahamu mwanamme,
lakini kuwa pia na mwanamke:
Ipokee dunia nzima mikononi mwako
Ukiipokea dunia basi Tao haitaondoka tena kwako nawe utakuwa kama mtoto mdogo.

Ijue rangi nyeupe,
lakini bakia na rangi nyeusi.
Kuwa mfumo kwa dunia,
Ikiwa wewe ni mfumo kwa dunia basi Tao itakuwa imara ndani yako na hakuna chochote utakachoshindwa kukifanya katika dunia hii.

Yajue yale ya kibinafsi,
lakini bakia na yale yasiyo na mahusiano na yeyote:
Ipokee dunia kama ilivyo
Na kama utaikubali dunia basi Tao itakuwa ikiwaka ndani yako na utarejea kuwa kile unachostahili kuwa.

Dunia huumbwa kutoka kwenye ombwe,
kama vifaa kutoka kwenye pande la gogo.
Gwiji anavielewa vifaa na umuhimu wake,
lakini bado anabakia na gogo lake.
Kwa hiyo anaweza akatumia au kutengneza vitu vyote.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

029

Unataka kuiboresha dunia ?
Ninadhani hilo haliwezekani.

Dunia ni takatifu mno.
Haiwezi kuboreshwa na kiumbe.
Ukicheza nayo utaiharibu.
Ukiichukulia kama kitu basi utaipoteza.

Kuna wakati wa kuwa mbele, na kuna wakati wa kuwa nyuma;
Wakati wa kutembea na wakati wa kusimama;
Wakati wa kuchakarika, kutumia musuli na kumwaga jasho na wakati wa kuchoka na kupumzika;
Wakati wa kuwa salama na wakati wa kuwa katika hatari.

Mwalimu huyaona mambo kama yalivyo, bila ya kutaka kuingilia kati wala kuyadhibiti.
Huyaachia yafuate mkondo wake yenyewe, wakati akiishi katikati ya duara la Tao.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

030

Anayeitegemea Tao kuwatawala binadamu huwa halazimishi jambo lolote au kuwashinda maadui kwa kutumia uongo au dhuluma au silaha.
Kwa kila nguvu inayotumika kuna nguvu kama hiyo hiyo ikiipinga nguvu hiyo ya kwanza.
Vitendo vyote vya kutumia nguvu hata iwe kwa nia njema kiasi gani bado siku zote humgeukia mtumia mabavu.

Gwiji huifanya kazi yake ni kisha husimama.
Anaelewa kwamba ulimwengu milele haudhibitiki, na kwamba ukiritimba na kujaribu kutawala kila kitu huenda kinyume na mkondo wa Tao.
Kwa sababu mwenyewe anajiamini huwa hana muda wa kuwafanya wengine wamwamini.
Kwa sababu anaridhika na kile alicho hana sababu ya kupata ridhaa ya wengine.

Kwa sababu anajikubali yeye mwenyewe, basi dunia nzima inamkubali.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

031

Silaha ni zana za maangamizi na watu wote wema huzichukia.

Silaha ni vifaa vya kuwatisha na kuwaogopesha watu, na kila mtu mwema hatozitumia isipokuwa pale ambapo haiwezekani kuacha kufanya hivyo,
na akilazimika kuzitumia, huzitumia kwa uangalifu mkubwa na kwa uzito na majonzi makubwa moyoni.

Amani ndicho kitu bora zaidi na cha thamani kubwa kabisa.
Amani ikitoweka ni vipi yeye ataridhika ?
Maadui zake si mazimwi, ila tu watu kama yeye mwenyewe alivyo.
Hawatakii mabaya.
Wala haushangili ushindi dhidi yao.

Atakuwaje na furaha ya ushindi na uchinjaji watu kama yeye ?

Huingia vitani kwa huzuni,
majonzi mengi na huruma kama vile mtu aendavyo mazishini.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

032

Tao haionekani.
Ndogo kuliko elektroni
na ndani yake ina dunia zisizo na idadi.

Kama wanaume na wanawake wenye nguvu wangelijikita kwenye Tao basi kila kitu duniani kingekuwa na upendo na amani.
Dunia ingelikuwa katika maridhiano.
Watu wote wangelikuwa katika amani, na sheria zote zingekuwa zimeandikwa katika mioyo yao.

Unapokuwa na majina na maumbo kumbuka hivi ni vitu vya muda.
Unapokuwa na taasisi weka mipaka ya mwisho wa shughuli zao.
Kujua wapi pa kuishia kutakusaidia kuepuka hatari na hasara nyingi.

Vitu vyote duniani huishia kwenye Tao, kama vile mito yote inavyoishia baharini.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

033

Kuwajua wengine ni kuwa na akili,
lakini kujijua mwenyewe ni busara na hekima.
Kuwaamuru wengine ni nguvu na uwezo,
kujiamuru mwenyewe ni dhima na mamlaka.

Ukitambua una kila kitu unachokihitaji katika maisha yako, basi hakika wewe ni tajiri.
Ukikaa katikati na kukumbatia umauti basi budi utaishi milele.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

034

Tao inasambaa kote.
Vitu vyote huzaliwa kutokana nayo, ingawa siyo inayoviumba,
Hujizatiti katika kazi yake,
lakini haina madai yoyote.
Huzilisha dunia nyingi tu, lakini haizimiliki.
Kwa kuwa inaungana na dunia zote na kujificha katika mioyo yao inaweza ikaitwa yenye nyenyekevu.
Kwa kuwa vitu vyote huishia ndani yake, nayo pekee ndiyo inayobakia
inaweza kutukuzwa na kuitwa maarufu.
Haina habari na umashuhuri wake, na hivyo kwa kweli ni maarufu sana.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

035

Yule anayejikita kwenye Tao anaweza kwenda mahala popote anapotaka bila kuogopa hatari yoyote.

Huuona umoja wa dunia, hata katika adha na maumivu makubwa kiasi gani,
kwa sababu ameshaipata amani katika moyo wake.

Muziki na harufu ya chakula kizuri huwenda vikawasimamisha watu kwa muda wakavifurahia.
Ila maneno yanayoelekeza watu kwenda kwenye Tao yanaonekana ni yale yale yanayojirudia na hayana ladha tamu.
Ukiitafuta huna utakachokiona.
Ukijaribu kuisikiliza huna utakachokisikia.
Ukiitumia, basi huwa haiishi.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

036

Ukitaka kukifanya kitu kiwe kidogo zaidi, lazima kwanza ukiachie kukua au kupanuka.
Ukitaka kukiteketeza kitu chochote ni lazima ukiachie kwanza muda wa kukua na kustawi.
Ukitaka kuchukua kitu chochote, lazima kwanza uwezeshe kitu hicho kutolewa.
Hili huitwa onekano yakinifu la jinsi mambo yalivyo.

Laini hushinda kigumu.
Na mwenda polepole humshinda mwenda mbio.
Fanya kazi yako iwe siri,
waoneshe watu kile ulichokwisha kukifanya.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

037

Tao huwa haifanyi kitu chochote,
lakini kupitia kwake vitu vyote hufanyika.

Kama wanawake na wanaume wenye nguvu wangeliweza kujiweka ndani yake,
Dunia nzima itabadilika yenyewe katika mdundo wake wa kawaida.
Watu wataridhika na maisha yao ya kawaida ya kila siku, katika maridhiano na bila matamanio yoyote.

Pakiwa hakuna matamanio basi dunia yote huwa katika amani.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

038

Mwalimu huwa hajaribu kuwa mtu mwenye nguvu au mamlaka,
Kwa hiyo ni mwenye nguvu na mamlaka kweli kweli.
Binadamu wa kawaida sikuzote hutaka kuwa na nguvu na vyeo zaidi;
Na kutokana na hili hata siku moja hawi na nguvu za kutosha wala hapati cheo cha kumridhisha.

Mwalimu kwa kawaida huwa hafanyi lolote,
Na bado huwa haachi lolote ambalo halijafanyika.

Mtu mwenye huruma hujitahidi kufanya chochote,
Lakini kunakuwa na mengi ambayo bado hayafanyiki.
Mtu muadilifu hufanya kitu fulani,
Lakini bado huwa anaacha mengi hayajafanyika.
Mtu mwenye utu hufanya kifu fulani, lakini pale anapoona hakuna kinachoendelea hukunja uso na mikono ya shati lake na kuanza kutumia nguvu.

Tao inapopotea basi wema hupatikana.
Wema nao unapopotea
basi utu huonekana.
Na utu unapopotea basi panakuwepo na mazoea.
Mazoea ni chuya za mazoea ya kweli,
Mwanzo wa vurugu na matatizo.

Kwa hiyo Mwalimu huwa anajishughulisha sana na vilivyo ndani zaidi na sio vilivyo juu au usoni.
Na tunda lenyewe na sio maua yake.
Hana dhamira binafsi.
Husihi katika uhalisia,
na huachia ndoto na mataminio yote kutoweka.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

039

Katika umoja na Tao mbingu ziko wazi na zina nafasi kubwa na ya kutosha,
Ardhi ni ngumu na iliyojaa,
Viumbe wote hustawi pamoja,
Wote wakiridhika kwa namna walivyo,
Daima dawamu wakijirudia wao wenyewe, bila mwisho wakizaliwa upya.

Mtu anapoiingilia Tao,
Anga hugeuka kuwa chafu,
Na ardhi huwa mashimo maltupu
Uwiano huporomoka
na viumbe hutoweka.

Mwalimu huangalia kila sehemu kwa huruma
kwa sababu anaelewa kilicho kizima.
Matendo yake ya kila siku ni unyenyekevu.
Hang'ari kama kito bali huiachia Tao kumuumba na kumfanya alivyo, asiye na umbo wala ulaini kama vile mawe ya kawaida.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

Sunday, September 5, 2010

040

Kurudi ndio mwendo wa Tao
Na kujisalimisha ndio njia ya Tao.

Kila kitu huzaliwa na kuwepo,
Kuwepo huzaliwa na kutokuwepo.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

040

Kurudi ndio mwendo wa Tao
Na kujisalimisha ndio njia ya Tao.

Kila kitu huzaliwa na kuwepo,
Kuwepo huzaliwa na kutokuwepo.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

041

Mtu bora anaposikia kuhusu Tao,
Hapo hapo huanza huikumbatia.
Mtu wa kawaida anaposikia juu ya Tao,
huamini nusu, na nusu huishuku.
Mtu mjinga anaposikia kuhusu Tao,
Hucheka kicheko kikubwa,
Kama asingelicheka, basi hii isingelikuwa ni Tao.

Ndio maana husemwa:
Njia ya kwenda kwenye mwanga huonekana ni yenye kiza,
Na njia inayompeleka mtu mbele aghalabu honekana kurudi nyuma,
Njia iliyonyooka huonekana refu,
Nguvu huonekana unyonge,
Utakatifu huonekana uchafu,
Kutobadilika huonekana kuwa kitu kinachowezekana kubadilika,
Uwazi huonekana kitu kilichofichika,
Mashuhuri huonekana watu wa kawaida,
Pendo kubwa na lisilo na ukomo huonekana kutokujali,
Na hekima iliyo kubwa huonekana kama mambo ya kitoto.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

042

Tao huzaa Moja.
Na Moja huzaa Mbili.
Mbili huzaa Tatu.
Na Tatu huzaa vyote vilivyomo duniani.

Vitu vyote vinaupa mgongo jinsia ya kike na husimama kuelekea jinsia ya kiume.
Jinsia ya Kike na Kiume zikichanganyika maelewano na amani hupatikana.

Mtu wa kawaida huchukia Utawa.
Mwalimu anaupenda na kuutumia, akakumbatia upweke akijua fika kwamba wakati huo yeye ni mmoja na ulimwengu wote.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

043

Kitu kilicho mororo kuliko vyote duniani hushinda kile kilicho kigumu kushinda vyote duniani.
Kile kisicho na kitu huingia ndani ya kile kisicho na nafasi.
Hili hudhirisha thamani ya dhana ya kutokufanya kitu.

Kufundisha bila ya maneno,
Kufanza bila ya kufanya kitu:
Hiyo ndiyo njia ya Mwalimu.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

044

Umaarufu au uadilifu ni kipi kilicho bora ?
Fedha au Furaha: ni kipi chenye thamani zaidi?
Kufaulu au Kushindwa: ni kipi kinachoharibu zaidi?

Ukijifananisha na wengine ili kukamilisha furaha yako,
milele hautokamilisha furaha hiyo.
Ikiwa furaha yako inategemea fedha,
haitokaa uridhike kwenye nafsi yako na kuwa na furaha.

Tosheka na kile ulicho nacho.
Ridhika kwa namna vitu vilivyokuwa,
Unapoona huna kitu unachokikosa basi dunia nzima huwa ni yako.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

045

Ukamilifu wa kweli huonekana una mapungufu,
hali ya kuwa ndio ukamilifu wenyewe.
Kujaa kikweli kweli huonekana kitu kitupu,
hali ya kuwa kimejaa mpaka juu.
Kilichoonyoka hasa, huonekana kupinda.
Busara ya kweli huonekana ujinga.
Na sanaa ya kweli huonekana takataka.

Mwalimu huachia vitu vitokee vyenyewe.
Huumba matukio kwa jinsi yanavyotokea.
Hujiweka pembeni na kuiachia Tao kujizungumza yenyewe.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

046

Nchi inapokuwa na maridhiano yenyewe kwa yenyewe,
basi viwanda hutengeneza malori na matrekta.
Wakati nchi naenda kinyume cha Tao
mabomu na makombora hulundikana kwenye viunga vya miji mikubwa ya nchi hiyo.

Hakuna kitu kisicho cha kweli kama vile UOGA,
na hakuna kosa kubwa kama kuanza kujiandaa kujilinda wewe mwenyewe,
na hakuna nuksi kubwa kama kuwa na adui.

Yeyote anayeweza kuona hadi ndani ya uoga sikuzote atakuwa salama.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

047

Bila kufungua mlango wako,
unaweza kufungua moyo wako kwa dunia nzima.
Bila kutazama dirishani mwako bado unaweza kuona chanzo cha Tao.

Kadri unavyojua mengi
ndivyo utakavyokuwa hauelewi.

Mwalimu hufika bilal ya kuondoka, huona mwanga bila ya kuangalia, na hufanikisha bila ya kutenda kitu chochote.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

048

Katika kutafuta elimu kila siku kuna kitu kipya kinachoongezwa.
Katika matendo ya Tao, kila siku kuna kitu kinachoondolewa.
Unahitaji kidogo na kidogo zaidi kuvilazimisha vitu, hadi hatimaye kufikia hali ya kutokufanya kitu.
Pale ambapo hakuna kinachofanyika,
basi sikuzote huwa hakuna kinachosahaulika kufanyika.

Ugwiji wa kweli hupatikana kwa kuachia mambo yajiendee yenyewe.
Hauwezi kupatikana kwa kuyaingilia mambo hayo.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

049

Mwalimu hana akili yake mwenyewe,
huwa anafanya kazi na akili za watu wengine.
Ni mwema kwa watu waliokuwa wema.
Ni mzuri pia kwa watu wasiokuwa wema.
Huu ndio wema wa kweli.

Huwaamini watu wanaoaminika.
Aidha, huwaamini pia watu wasioaminika.
Huu ni uaminifu wa kweli.

Akili ya Mwalimu ni kama anga za juu.
Hakuna anayemwelewa.
Humuangalia na kusubiri.
Naye huwachukulia watu kama watoto wake.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

050

Mwalimu huwa anajitolea kwa lolote lile linalokuja mbele yake wakati wowote.
Anajua alizaliwa na atakufa,
na hakuna atakayemnusuru na hilo:
Hana kinachomdanganya akilini mwake
na hakuna kizuizi katika mwili wake.
Hakai kufikiria kile anachokitenda
Maana matendo yake huwa yanatiririka kwenye kiini cha ndani cha utu wake.
Huwa hazuii kitu chochote katika maisha yake;
Kwa hiyo yuko saa zote tayari kwa mauti.
Kama mtu anavyokuwa tayari kwenda kulala
baada ya kazi nzuri kwa siku hiyo.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

051

KIla kiumbe ulimwenguni ni taswira ya Tao.
Huwa hai ghafla
bila kujijua, iliyokamilika na huru.
Kisha huchukua umbo la kiumbe na kisha kuachia mazingira kuikamilisha.
Ni kwa sababu hii ndio maana kila kiumbe huitukuza Tao papo kwa hapo kinapozaliwa.

Tao ndio inayozaa viumbe wote,
Huwalisha,
Huwakimu, Huwatunza, Huwaliwaza, Huwalinda, na huwarudisha kwake yenyewe, huumba bila kumiliki, hufanza bila kutarajia, huongoza bila kuingilia.
Hii ndiyo sababu mapenzi kwa Tao yamo katikati ya asili ya kila kitu.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

052

Hapo mwanzo kulikuwa na Tao
Vitu vyote hutoka na kisha kurudi tena kwenye Tao.
Ili kujua asili ya kitu fuatilizia kwanza kuwepo kwake.
Unapowatambua watoto na kumuona mama yao,
huo utakuwa ni mwisho wa huzuni yako.

Ukiwa unawahukumu wengine duniani,
Na ukaanza kucheza na matamanio moyo wako utaanza kusumbuka.
Ikiwa hauwahukumu wengine na haauongozwi na matamanio yako basi moyo wako utakuwa katika amani.

Kuona katika giza ni ubayana.
Na kujua wakati wa kujisalimisha ni nguvu na uwezo.
Tumia mwanga wako mwenyewe ili urudi kwenye chanzo cha mwanga.
Hili linaitwa ni kufanya mazoezi ya utu wa milele.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

053

Njia hii kuu ni rahisi,
hata hivyo watu hupendelea vichochoro.
Tambua ni wakati gani mambo hayana ulingano. Jitahidi uwe katikati mwa Tao.

Walanguzi matajiri wanaponeemeka
Wakati wakulima wanadhulumiwa ardhi yao;
wakati maofisa serikali wanapotumia fedha kununua silaha badala ya kununua dawa;
wakati tabaka la juu ni wabadhirifu na mafisadi na masikini hawana pa kukimbilia-haya yote ni wizi na rabsha.
Huu kamwe si mwenendo unaoendana na Tao.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

054

Kila aliyepandwa katika Tao
hawezi kung'olewa tena.
Kila anayekumbatia Tao hawezi tena kuteleza na kuanguka.
JIna lake litatukuzwa kwa hesima toka kizazi kimoja hadi kizazi kingine.

Acha Tao iwe katika maisha yako ya kila siku nawe utakuwa mkweli na halisi.
Acha Tao iwe katika familia yako na familia yako itafaulu na kufanikiwa katika kila jambo.
Acha Tao iwe katika nchi yako na nchi yako itakuwa mfano wa kuigwa na mataifa mengine duniani.
Acha Tao iwe katika ulimwengu na ulimwengu utaimba.

Ninajuaje haya ni kweli ?
Ni kwa kuangalia kilichoko ndani mwangu.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

055

Yule anayeoana na Tao ni kama vile mtoto mdogo aliyezaliwa jana.
Mifupa yake ni laini, na musuli zake ni dhaifu
lakini kamata yake ina nguvu ya kutisha.
Huwa hakajui lolote kuhusu kujamiana, lakini la kushangaza ni kwamba kaboo kake husimama,
Ana uwezo wa ajabu na unaotisha kiasi ambacho aweza kwa siku nzima kulia na kutoa kelele inayosikika mbali sana,
Lakini sauti yake haikauki
Utulive wake umekamilika mno.

Uwezo na nguvu ya gwiji ni kama hivi:
Huviachia vitu na watu wote waje kwake na kisha waondoke bila kuwa na matamanio yoyote.
Huwa hategemei matokeo
kwa hiyo hawezi akasikitika.
Kwa kuwa si mtu wa kusikitika basi huwa utu wake hauzeeki kamwe.


AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

056

Wanaojua huwa hawasemi.
Wanaozungumza sana huwa hawajui.

Funga mdomo wako,
zitie ganzi hisia zako,
Tia ubutu makali yako,
Yafungue mafundo yako
Lainisha mtazamo wako,
Ketisha chini vumbi lako,
Huu ndio utambulisho wa msingi.

Kuwa kama Tao.
Hauwezi kuifuata wala huwezi kuikimbia,
Kunufaika au kudhurika,
kutukuzwa au kudhalilishwa,
Huwa yajitolea mhanga wakati wote.
Ni kutokana na hili ndio maana hudumu milele.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

057

Ikiwa unataka kuwa kiongozi bora,
Lazima ujifunze kwanza kuifuata Tao.
Acha kutaka kudhibiti.
Achana na mipango isiyobadilika na dhana tasa,
Na dunia yako itaanza kujitawala yenyewe.

Kadri ulivyo na vikwazo na vizuizi vingi,
Ndivyo utakavyokuwa na watu wengi wasio waadilifu.
Kadri utakavyokuwa na silaha nyingi,
Ndivyo watu watakavyozidi kujiona sio salama.
Kadri unavyotoa ruzuku nyingi,
Ndivyo wananchi wanavyokuwa wategemezi zaidi.

Kwa hiyo gwiji hubainisha:
Huwa ninaachana na sheria,
Na ndivyo watu wanavyokuwa waaminifu zaidi.
Huwa ninaachana na uchumi,
na ndivyo watu wanavyofanikiwa kiuchumi zaidi.
Huwa ninaachana na dini,
Na ndivyo watu wanavyokuwa watulivu zaidi.
Huwa ninaachana na matamanio yote kwa manufaa ya walio wengi,
Na manufaa haya husambaa kila mahala kama majani.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

058

Nchi inapotawaliwa kwa uvumilivu mkubwa,
Watu hustarehe na huwa waaminifu.
Nchi inapotawaliwa kwa kuwakandamiza watu na kuwaficha ukweli watu hukata tamaa na huwa wajanja kupita kiasi.

Uchu wa madaraka na kutaka kutawala unapokithiri,
Na malengo na matarajio yanapokuwa makubwa, basi na matokeo kiufanisi huwa sawa na hamna.
Jaribu kutengeneza mazingira ya watu kuwa na raha na furaha,
Kama hutakuwa unajenga msingi wa dhiki na matatizo chungu nzima.
Jaribu kufanya watu wawe watakatifu,
Na hujenga msingi wa jamii ya watu waovu, wezi na wazinzi.

Kwa hiyo Mwalimu huwa mtu anayetosheka kuwa mfano kwa wengine bila ya kutaka ukuu.
Ana ncha kama mkuki lakini hatoboi kitu.
Kanyooka, lakini teketeke.
Ana nuru kali, lakini hayaumizi macho ya watu.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

059

Hakuna kilicho bora katika kutawala nchi kama vile kiongozi kuwa mtu wa kiasi.

Alama ya mtu wa kiasi ni ile ya mtu kuwa huru kutoka fikira zake mwenyewe.
Mvumilivu kama mbingu,
Na anayepenya kila kitu kama vile miale ya jua,
Imara kama mlima
Na mwepesi kama mti kwenye kimbunga,
Hana kwa wakati huo anakokwenda,
Na huridhika kutumia chochote anacholetewa na maisha.

Hakuna kinachoshindikana kwake.
Kwa sababu ameachia kila kitu anaweza kuiangalia jamii nzima kama vile mama anavyomtunza na kumlea mwanawe.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

Saturday, September 4, 2010

060

Kutawala nchi kubwa
Ni sawasawa na kukaanga samaki mdogo.
Humharibu samaki kwa kumgusa gusa sana.

Iweke nchi yako katikati ya Tao
Na maovu hayatakuwa na mwanya.
Sio kwamba kwa sababu maovu hamna
Ila ni kutokana na ukweli kwamba utaweza kuyakwepa kirahisi.

Usiachie uovu ushindane na mtu au kitu chochote
Na wenyewe hatimaye utatoweka.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

061

Nchi moja inapokuwa na nguvu sana duniani, hushabihiana na bahari.
Mito na vijito vyote hutiririsha maji yajaye humo.
Kadri inavyokuwa na nguvu zaidi ndivyo inavyopaswa kuwa na unyenyekevu zaidi.
Unyenyekevu una maana ya kuiamini Tao zaidi,
hivyo kutokuwa na haja ya kujihami.

Taifa kubwa ni kama vile mtu maarufu,
Anapofanya kosa haraka hutambua makosa yake.
Anavyotambua kafanya kosa hukiri kufanya kosa.
Akishakubali kosa lake haraka hujisahihisha.
Huwahusudu na kuwathamini wale wanaoonyesha udhaifu wake
kwani huwachukulia kama walimu wake walio wema sana kwake.
Huwachukulia maadui zake kama kivuli chake mwenyewe.


Taifa huwa limejikita kwenye Tao
pale linapowaruzuku vyema watu wake na haliingilii mambo ya watu wengine,
litakuwa ni mwanga kwa mataifa mengine duniani.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

062

Tao ndio kitovu cha ulimwengu,
hazina ya mtu mwema,
na hifadhi ya mtu mwovu.

Nishani huweza kununuliwa kwa maneno mazuri,
na heshima hupatikana kwa matendo mema;
Lakini Tao imezipita thamani zote,
na hakuna amayeweza kuipata.

Kwa hiyo, kiongozi mpya anapochaguliwa usijitolee kumsaidia kwa mali yako au kwa utaalamu ulio nao.
Badala yake jitolee kumfundisha nini maana ya Ta0.

Kwanini watu wa kale waliheshimu sana Tao ?
Kwa sababu ukiwa miongoni mwa wenye kuienzi Tao
Ukitafuta hupata;
na unapofanya kosa husamehewa.
Hii ndio sababu kila mtu anaipenda Tao.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

063

Tenda bila ya kufanya;
Fanya kazi bila kufanya lolote.
Ona jambo dogo kama vile ni jambo kubwa
na vitu vichache kama vingi.
Kabili jambo ligumu wakati bado ni jepesi;
Fanikisha mambo makubwa
kwa kupiga hatua moja ndogo baada ya nyingine.

Gwiji hahangaiki kufikia ukubwa; na ndio maana anakuwa mtu mkubwa.
Anapokumbana na matatizo,
huacha kuendelea na kuukabidhi moyo wake.
Hang'amg'abni kona yake ya starehe,
ma hivyo kwake tatizo sio tatizo.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

064

Kilicho na mizizi ni rahisi kupata lishe bora.
Kilicho bado kipya ni rahisi kusahihisha.
Kilicho kigumu ni rahisi kuvunjika.
Kilicho kidogo ni rahisi kukitawanya.

Zuia rabsha kabla haijaanza.
Panga vitu uzuri kabla havijakuwepo.
Mti mkubwa wa msonabari huanza kama mchicha dhaifu.
Safari ya maili elfu moja huanza chini ya miguu yako.

Kukimbilia kuanza kufanya jambo huishia kushindwa.
UKijaribu kuvikamata vitu huishia kuvipoteza.
UKikimbilia kukamilisha mradi huishia kuharibu kilichokuwa kimekwiva tayari.

Kwa hiyo gwiji hutekeleza mambo kwa kuachia yafuate mkondo wake yenyewe.
Huwa mtulivu yanapofikia mwisho kama alivyokuwa wakati yakianza.
Hana chochote, kwa hiyo hana lolote la kupoteza.
Alicho na ashiki nacho ni kukosa ashiki.
Anachojifunza ni kufuta alichokwishajifunza.
Huwa anawakumbusha watu kile tu ambacho tayari walishakuwa sikuzote.
Hana kingine anachokijali ila Tao tu.
Kwa hiyo anaweza kuvijali na kuviangalia vitu vyote.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

065

Magwiji wa kale hawakujaribu kuwaelimisha watu, ila kwa wema kabisa waliwafundisha kutokufahamu.

Watu wanapofikiri kuwa tayari wanajua majibu ya mambo yote wanakuwa wagumu kuelekezwa.

Wanapokuwa wanajua kuwa hawajui inakuwa ni rahisi kwa watu kujiongoza wao wenyewe.

Ikiwa unataka kujifunza kutawala, epuka kuwa mwenye akili sana au tajiri.
Mfumo rahisi kabisa ndio ulio dhahiri na wazi zaidi.
Tosheka na maisha ya kawaida,
unaweza kumuonesha watu wote njia ya kurudi kwenye asili yao ya kweli.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

066

Mito yote huelekea baharini
kwa kuwa iko chini kuliko ilivyo mto.
Unyenyekevu wake ndio huipa nguvu iliyokuwa nayo.

Ukitaka kutawala watu
ni lazima wewe ujiweke chini yao.
IKiwa unataka kuwaongoza watu,
ni lazima ujifunze jinsi ya kuwatii na kuwafuata.

Gwiji daima yuko juu ya watu,
na hakuna anayejisikia anakandamizwa.
Huwatangulia watu wake kwa kila jambo, na hakuna anayejisikia kwamba anatumiwa.
Dunia nzima huwa inamshukuru.
Kwa kuwa hashindani na mtu, hakuna anayeweza kushindana naye.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

067

Kuna wanaosema mafudisho yangu eti ni ujinga.
Wengine wanasema ni aali lakini yasiyotekelezeka.
Lakini kwa wale waliobahatika kujitazama ndani mwao;
huo ujinga una maana kamili inayoeleweka.
Na kwa wanayoyatia katika vitendo
huu uaali una mizizi inayoingia ndani sana.

Nina vitu vitatu tu vya kufundisha:
Kutokujiona, Uvumilivu na Huruma.
Hivi vitatu ni hazina yako iliyo bora kabisa.
Kutokujiona katika matendo na mawazo,
kunakurudisha kwenye chanzo cha kuwepo kwako.
Uvumilivu na rafiki na maadui zako unakubaliana na hali halisi kama ilivyo.
Huruma kwa upande wako mwenyewe, unapatanisha vitu vyote duniani.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

068

Mwanariadha bora
hupenda mshindani wake awe katika kiwango chake cha juu.
Jemadari bora huingia akilini kwa adui yake.
Mfanyabiashara mkubwa na anayefanikiwa sana huwa anatumikia maslahi ya jamii yake.
Na kiongozi bora huwa anafuata matakwa ya wale anaowaongoza.

Wote huwa wanaenzi maadili ya kutokuwa na ushindani.
Sio kwamba hawapendi kushindana,
ila hushindana katika mazingira ya kimchezo na utani.
Katika hili hakika ni sawa na watoto
na hawapingani kabisa na Tao.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

069

Majemedari wana msemo kwamba:
"Kuliko kuanza wewe kushambulia, ni bora zaidi wewe kusubiri na kuona.
Kulikoni kusogea hata nchi moja
ni bora kurejea nyuma hata kwa zaidi ya yadi moja.

Hili huitwa kusonga mbele bila ya kusogea mbele,
kurudisha nyuma bila ya kutumia silaha.

Hakuna nuksi kubwa kama kumdharau mpinzani wako.
Kumdharau adui yako ina maana kwamba wewe unaamini yeye ni mwovu.
Kwa hiyo unaziteketeza hazina zako tatu bora na kujigeuza wewe mwenyewe adui.

Pande mbili za wababe zikikutana kwenye kitali,
ushindi kwa kawaida huwa unakwenda kwa yule anayejua na anayekubali kushindwa.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

070

Mafundisho yangu ni rahisi kuelewa na ni rahisi kuyatia katika vitendo.
Hata hivyo ubongo wako hauwezi kamwe kuyaelewa,
na ukijaribu kuyatia katika vitendo lazima utashinwa.

Mafundisho yangu ni ya zamani kuliko dunia.
Utawezaje kiumbe kuelewa maana yake ?

Ikiwa unataka kunijua mimi,
jiangalie ndani ya moyo wako.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

071

Kutokujua ndio pekee maarifa ya kweli.
Kujifanya unajua ni maradhi.
Kwanza tambua wewe ni mgonjwa:
na kisha unaweza kuelekea kwenye afya na uzima.

Gwiji ni tabibu kwake yeye mwenyewe.
Amekwishajiponya na kujua kwa aina zote.
Kwa hiyo ni mzima kamili.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

072

Wakishaachwa kushangaza na watu na vitu,
watu hukimbilia kwenye dini.
Wakati huwa hawawezi tena kujiamini,
huanza kuitegemea serikali.

Kwa hiyo gwiji hurudi nyuma
ili watu wasichanganyikiwa.
Huelimisha bila ya kufundisha,
ili watu wasiwe na chochote cha kujifunza.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

073

Tao sikuzote imo katika utulivu.
Hushinda bila ya kulazimisha,
hujibu bila kutamka neno hata moja,
huwasili bila ya kuitwa.
na hutekeleza bila kuwa na mpango.

Nyavu zake hugubika dunia nzima;
Na ingawa matundu yake ni mapana,
huwa haiachii hata kitu kimoja kuponyoka.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

074

IKiwa utamaizi kila kitu hubadilika, hakuna utakachojaribu kuking'ang'ania.
Kama haugopi kufa,
hakuna utakachoshindwa kukifanya.

Ukijaribu kuidhibiti akheri,
ni kama kutaka kuchukua nafasi ya seremala gwiji.
Ukizishika zana za serelamala gwiji, uwezekano ni kuwa lazima utajikata mkono wako.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010

075

Kodi zinapokuwa juu sana,
watu hulala na njaa.
Serikali ikiwa kizabizabina na kuingilia
sana mambo ya watu watu hupoteza imani yao.

Fanza jambo kwa manufaa ya watu.
Waamini, na kisha waache peke yao.

AYA ZA MTAWA
[ Tao-Te-Ching ]


Copyright © Sammy Makilla-2010